bofya hapa kudownload historia ya muungano
MUUNGANO kati ya Tanganyika na Zanzibar ndio uliozaa nchi inayoitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Hata
hivyo muungano huo ulioasisiwa na Hayati Mwalimu Julius Nyerere na
Hayati Abeid Karume, umekuwa ukihojiwa mara kwa mara kutokana na kasoro
nyingi zilizomo.
Baadhi ya Wazanzibari wamezibainisha kasoro zilizomo kwenye muungano huo na kushauri kufanyika kwa tathmini ya muungano uliopo.
Mkataba wa Zanzibar katika muungano uko wapi?
Kundi
la Wazanzibari 15 maarufu kama G15 ni kati ya makundi mbalimbali
vinavyojitokeza kuhoji uhalali wa muungano huku vingine vikishia
kuishitaki serikali mahakamani.
Kundi hilo limejitokeza tangu
mwaka 2005 ambapo liliishitaki Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ili kupata
mkataba huo. Ndipo ofisi ya Mwanasheria mkuu wa Zanzibar ilipokiri
kutokuwa na mkataba huo.
Mwaka 2010 kundi hilo liliandika barua Umoja wa Mataifa kutaka muungano huo ufanyiwe tathmini upya.
Mbali
na Umoja wa Mataifa, wamepeleka nakala ya barua hiyo katika balozi za
nchi za Marekani, Uingereza, Urusi, Ufaransa, Ujerumani na Umoja wa Nchi
huru za Afrika.
Makamu mwenyekiti wa G 15, Rashid Yusuf Mshenga
anasema kuwa Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar haukuwa na uhalali
kwakuwa Zanzibar hawakupewa mkataba.
“Muungano huu ni ‘verbal’
tu, ni wa kuchanganya mchanga tu wan chi mbili, lakini ukiuliza Mkataba
wa muungano haupo. Tunataka muuungano huu upitiwe upya,” anasema
Mshenga.
Anasema kuwa upande wa Tanzania bara walipata mkataba wa
Muungano uliokuwa umesainiwa, lakini upande wa Zanzibar mkataba huo
haukupatikana hali inayotia shaka katika muungano,
“Wenzetu bara,
Spika wa kwanza Adam Sapi Mkwawa na Pius Msekwa walibaki na nakala ya
Mkataba, lakini Zanzibar hadi leo haupo, wala hakukuwa na Barza la
Mapinduzi lililokaa kujadili muungano. Hata Mzee Aboud Jumbe alipoingia
madarakani alikiri kuwa hakukuwa na mkataba” anasema.
Mshenga
ameshangazwa na Serikali ya Muungano na SMZ kuweka kamati ya
kushughulikia kero za Muungano wakati hata Mkataba wa muungano haupo
akisema kuwa hiyo ndiyo kero ya kwanza.
“Kamati ya kushughulikia
kero za muungano inaundwa na makada wa CCM, kama Waziri mkuu na viongozi
wa SMZ, wote hawawezi kuhoji mambo muhimu”.
Mshenga ameshauri
kuwa ili kupata uhalali wa Muungano, Serikali ya Muungano na serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar waunde timu za kuujadili muungano kasha iitishwe
kura ya maoni ili wananchi waamue muungano wanaoutaka.
Kwa upande
wake Nassor Hassan Moyo aambaye ni mmoja wa waasisi wa Mapinduzi ya
Zanzibar na muungano huo, ameshangazwa na madai kuwa Zanzibar haikupata
mkataba.
Anasema mkataba ni moja kati ya nyaraka muhimu za
serikali hivyo wanaopaswa kuwajibika ni Ikulu ya Zanzibar na ofisi ya
Mwanasheria.
Akieleza jinsi hatua za kuunganisha Tanganyika na
Zanzibar zilivyofikiwa, Moyo anasema kuwa muungano ulifanywa na
kiurafiki zaidi.
“Wakati ule Mwalimu Nyerere na Karume walikutana
kukubaliana kuungana. Baada ya makubaliano hayo, Mwalimu na ujumbe wake
wakiwamo Oscar Kambona, Bokhe Munankha, Job Lusinde na Ali Mwinyi
Tambwe walikuja Zanzibar na kusaini mkataba wa muungano. Kwa upande wa
Zanzibar walikuwapo Kassim Hanga, Abdulaziz Twala na Ali Mwinyigogo.
Baada
ya hapo Karume aliitisha Baraza la Mapinduzi na kutueleza. Tulimuuliza
baadhi ya mambo kama vile elimu ya bure, afya kama bado vitatolewa bure,
akasema vitaendelea hivyo na sisi tukaafiki” anasema Moyo.
Lakini Moyo anasema kuwa kwa wakati ule hakukuwa na mwamko mkubwa wa watu kuhoji mambo tofauti na sasa.
“Naunga
mkono vijana wanaohoji muungano, muungano ni wao, sisi muda wetu
umekwisha, wananchi wanahaki ya kuhoji uhalali wa muungano.” anasema
Moyo.
Huku akionyesha kuguswa na ibara ya 9(2) ya muswada wa
marejeo ya Katiba inayokataza wananchi kuyaondoa mambo muhimu kama vile
muungano, urais, uwepo wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na
mengineyo, Moyo alisema kuwa wananchi wasizuiwe kuyajadili mambo hayo.
“Kwa
sasa serikali inafanya jitihada za kurekebisha Katiba ambapo pia
muungano utaangaliwa. Lakini sasa wamezuia mambo muhimu kuzungumziwa.
Kwanini uwazuie watu kujadili muungano, kwanini wanasiasa wasishiriki
kwenye mchakato wa Katiba? Nyerere hakuwa askofu wala Karume hakuwa
mufti, wote walikuwa wanasiasa na ndiyo waliounda muungano, kwanini
wanasiasa wa leo wasiruhusiwe?” anasema Moyo.
Maswali mengi bila majibu
Kwa upande wake Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Othman Masoud Othman, anasema muungano una kasoro za msingi za kimaumbile.
Anazibainisha
kasoro hizo ambazo anasema ni miongoni mwa sababu za muungano kuwa na
kero sugu kuwa ni kuwepo kwa masuala ya msingi ya kikatiba ambayo
hayana majibu ama kutoka ndani ya Katiba, Sheria, Sera na hata kutoka
kwa watendaji.
Utata wa kwanza kwa mujibu wa Othman ni kama washiriki wa muungano bado wapo au hawapo?
“Kwa
vile nchi ambazo zimeungana kwa baadhi ya mambo tu, inategemewa kwamba
waliounganisha mambo hayo wapo, wana vikao rasmi vinavyotambuliwa na
Katiba na Sheria za Nchi.
Ilitegemea kuwa Washirika hao wanaamua
kuongeza kupunguza mambo ya Muungano wakiwa na nguvu sawa ya uamuzi.
Ilitegemea kuwa Washirika hao wana kauli sawa za maamuzi juu sera,
uendeshaji na Sheria za Muungano. Suala ni kuwa hivi ndivyo hali
ilivyo?” anahoji.
Kuhusu mambo ya muungano, Othman anajadili maana ya mambo ya muungano na idadi yake.
Anafafanua kuwa, jambo linapoitwa la Muungano ni kuwa Zanzibar haina uwezo wa kulisimamia kisera, kiutawala na kisheria.
“Hata
hivyo suala hili ni gumu kuliko linavyoonekana. Kabla ya kuja sera za
biashara Huria mashirika kama vile Air Tanzania, Shirika la Posta na
Simu na Benki ya Taifa ya Biashara na mengineyo yakijulikana kama
mashirika ya Muungano. Katika vikao kadhaa ilikubaliwa kuwa Zanzibar
ishirikishwe katika uendeshaji wa mashirika hayo ya Muungano. Mashirika
hayo mengi yamebinafsishwa” anasema Othman.
Kuhusu uwakilishi wa Zanzibar katika muungano
kupitia
Rais wa Zanzibar ambaye alikuwa Makamo wa Rais wa Muungano kwa kupitia
wadhifa wake wa Urais wa Zanzibar, Othman anajadili marekeisho ya 11 ya
Katiba ya Jamhuri ya muungano,
“Baada ya Marekebisho ya 11 ya
Katiba Rais wa Zanzibar aliondolewa katika nafasi ya Makamo wa Rais kwa
kupitia wadhifa wake. Badala yake Makamo wa Rais anapatikana na
utaratibu wa Mgombea Mwenza. Chini ya ibara ya 47(3) ya Katiba ya
Muungano, Mgombea Mwenza anateuliwa kwa Kanuni kuwa iwapo Rais ni mtu
anayetoka upande mmoja wa Jamhuri ya Muungano, Makamo wa Rais awe ni mtu
anayetoka upande wa pili wa Muungano”.
Kuhusu Uchumi, Othman
ananukuu Kitabu cha Muafaka baina ya SMT na SMZ kinachoeleza kuwa
“Tanzania ni nchi moja yenye uchumi mmoja wenye mazingira tofauti”,
lakini anasema katika utekelezaji Serikali zote mbili zinaonyesha kuwa
na jibu tofauti – kwamba uchumi wa Tanzania Bara na Zanzibar ni tofauti.
“Mtafaruku uliopo unatokana na ukweli kwamba ingawa chumi ni
mbili lakini nyenzo zote kuu za uchumi zinadhibitiwa na Serikali ya
Muungano. Nyenzo kama vile udhibiti wa sera za fedha, kodi na mahusiano
na nchi za nje hazimo mikononi mwa Zanzibar ingawa Zanzibar inategemea
ijiendeshe kiuchumi”.
Nini kifanyike?
Ili kuudumisha
muungano, Othman anasema kuwa hautalindwa kwa siasa na kuusifu pekee na
kuwaita wale wanaoukosoa kuwa ni maadui wa Muungano ingawa wapenzi wa
Muungano wenyewe wanazikubali kasoro hizo hizo na hata wameziandika na
kuzifanyia vikao.
“Muungano utalindwa kwa kuwekewa misingi
madhubuti iliyo wazi na ambayo italindwa kwa misingi ya Katiba na Sheria
inayokubalika na ambayo itatokana na ridhaa za washirika wa Muungano”.
Akitoa
mfano wa Uingereza na Scotland, Othman anasema kuwa kumekuwa na
marekebisho kadhaa ya kuboresha muungano wao, tofauti katika Muungano wa
Tanzania ambapo marekebisho mengi ya kikatiba, kishera na kisera
yanafanya Muungano kuwa na matatizo zaidi kwa vile kiini cha Kero za
Muungano hakijashughulikiwa. Maswali ambayo hayana majibu ni mengi
ndani ya Muungano.
“Hakuna Muungano madhubuti ambao unategemea
kulindwa na sera za chama. Muungano madhubuti ni ule unaolindwa na
misingi madhubuti, uwazi na wenye majibu kwa masuali yanayohusu nguzo
kuu za Muungano huo,” anasema Othman.
RATIBA NZITO YA SOKA HII LEO: MANCHESTER UNITED, ROMA, FENERBAHCE VITANI
-
*Leo hii kuna mechi kibao sana ambazo zitapigwa kule Uingereza pia kuna
mechi kali ya Derby Country atakiwasha dhidi ya Sheffield Wednesday kule
ugen...
1 hour ago







0 comments:
Post a Comment